Pages


Photobucket

Monday, October 29, 2012

SCANDINAVIA YAFUKUZWA KWA KUTOLIPA PANGO

Vifaa vya Ofisini mali kampuni ya Scandinavia Express vikiwa vimetolewa nje jijini Dar es Salaam jana. Vilitolewa na madalali wa mahakama kwa madai ya kushindwa kulipa mkopo ambao hata hivyo haikufahamika ni kiasi gani. Picha na Fidelis Felix
“Hii ni operesheni endelevu, kwa hiyo, wadaiwa wengine sugu wajiandae. Kama walijua kuwa Serikali hii haiwezi kuwachukulia hatua zozote, basi tutawaondoa wote bila kujali hadhi wala wadhifa wa mpangaji,” alitahadharisha Tarimo.

Kampuni ya Usafirishaji ya Scandnavia imetimuliwa katika majengo ilimokuwa imepanga kwa matumizi ya shughuli zake za kiofisi, kutokana na kushindwa kulipa kodi ya pango zaidi ya Sh200 milioni.

Kampuni hiyo iliyokuwa imepanga katika majengo yanayomilikiwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) yaliyoko Kariakoo eneo la Kamata, jijini Dar es Salaam, ilitimuliwa na TBA, katika operesheni inayoendeshwa na TBA dhidi ya wapangaji wake ambaoni wadaiwa sugu.

Mbali na Scandnavia, kampuni nyingine tatu ambazo ni jirani yake, zilizokuwa zimepanga katika majengo hayo ya TBA yaliyopo Kamata, pia zilitimuliwa kutokana na kushindwa kulipa kodi ya pango kwa muda mrefu.

Kampuni hizo zilizotimuliwa katika operesheni hiyo iliyoendeshwa chini ya ulinzi mkali wa askari Polisi wenye silaha, ni pamoja na Shems & Sons, Desktop Computers (kwa sasa Panorama Communications Institute) na Sky Net.

Mwananchi lilifika eneo la ofisi hizo zote mchana na kushuhudia samani na vifaa mbalimbali vya ofisi hizo vikiwa vimetapakaa nje, huku maofisa wa TBA wakiweka makufuli katika milango ya vyumba vilivyokuwa vinatumiwa kama ofisi za kampuni hizo.

Maofisa wa kampuni hizo walikuwapo eneo la tukio wakati hawakuwa tayari kuzungumza lolote, wakidai kuwa wao si wasemaji na kwamba wasemaji hawakuwepo na hawakujua walikokuwa wamekwenda.

Ofisa mmoja wa Kampuni ya Scandnavia ambaye hata hivyo hakutaka kujitambulisha alisema anayeweza kuzungumzia operesheni hiyo ni Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Mohamed Abood lakini akasema hayupo na wala hajui mahali alikokwenda.

Katika ofisi za Chuo cha Mawasiliano cha Panorama (Desktop) maofisa waliokuwapo waligoma kuzungumza lolote na kurushiana mpira huku wakidai kuwa mzungumzaji ambaye ni mmiliki wa chuo hicho alikuwa ametoka muda mfupi baada ya operesheni.

Ofisa Miliki wa TBA Erasmi Tarimo aliliambia Mwananchi kuwa Scandnavia inadaiwa kiasi cha Sh220 milioni, ambazo ni malimbikizo ya kodi ya pango ya miaka takribani minane.
Alisema kuwa kampuni hiyo inatakiwa kulipa kodi ya Sh3 milioni tu kwa mwezi, lakini imekuwa ikilimbikiza deni hilo hadi limefikia kiasi hicho.

Tarimo aliongeza kuwa kampuni hiyo pamoja na nyingine ambazo zilitupiwa virago jana licha ya kuandikiwa barua mara kadhaa kuzikumbushia kulipa deni lake lakini zimeshindwa kufanya hivyo.

“Tumeshawaandikia barua nyingi sana kuwakumbushia, wengine wamekuwa wakilipa kidogo kisha wanaendelea kulimbikiza na wengine hawajalipa kabisa. Katika hali kama hii inabidi hatua kama hizo zichukuliwe, na hata Sheria za Kodi zinaturuhusu kuwaondoa wasiolipa,” alisema Tarimo.

Akizungumzia operesheni hiyo, Tarimo alisema kuwa kwa jana ilifanyika katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam, kama vile Ilala, Mikocheni, Mbezi, Kurasini na kwingineko ambako kuna wadaiwa wake sugu.

“Hii ni operesheni endelevu, kwa hiyo, wadaiwa wengine sugu wajiandae. Kama walijua kuwa Serikali hii haiwezi kuwachukulia hatua zozote, basi tutawaondoa wote bila kujali hadhi wala wadhifa wa mpangaji,” alitahadharisha Tarimo.

Hata hivyo alisema kuwa operesheni hiyo jana iliendeshwa vizuri bila vipingamizi, kwa kuwa walipata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Jeshi la Polisi waliohakikisha usalama, Serikali za Mitaa na hata kwa wapangaji wenyewe.
Chanzo: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment