Pages


Photobucket

Thursday, November 1, 2012

ZITTO: SERIKALI ITOE MAELEZO YA SH BIL 25

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), ameitaka Serikali kufanya ukaguzi maalum wa kuchunguza ubadhirifu wa matumizi ya Sh bilioni 25, zilizotolewa na Serikali mwaka 2010/11, kwa ajili ya Wizara ya Fedha, mikoa na katika halmashauri.

Hatua ya Zitto, imekuja baada ya kutoridhishwa na majibu ya swali lake la msingi, yaliyotolewa bungeni mjini hapa jana na Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum.

Zitto alionyesha kushangazwa kusitishwa na kutokuwepo kwa maelezo ya matumizi halisi ya fedha hizo, katika taarifa ya Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali ( CAG), kutoandika taarifa juu ya matumizi ya fedha hizo.

Kutokana na hali hiyo, aliihoji Serikali kama iko tayari kufanya ukaguzi maalum, ili kubaini kama fedha hizo, zilitumika kwa matumizi yaliyotakiwa katika Wizara ya fedha, Halmashauri na mikoa kwani fedha hizo ni za umma, zimetumika sawasawa.

“Mimi nimehoji mwaka wa fedha 2010/11, ambao unaoishia Juni 2011, ila nimejibiwa kwa taarifa za 2011/12 mwezi agosti, ambao sio sahihi ndio maana nasema swali langu halijajibiwa,” alisema Zitto.

Alisema katika mwaka huo, Hazina ilitoa jumla ya Sh tirioni 9, kwa ajili ya kupeleka katika maeneo hayo, lakini katika fedha hizo jumla ya Sh bilioni 25, hazijulikani ziko wapi.

Alisema pamoja na taarifa ya CAG kutoonyesha matumizi ya fedha hizo, lakini hazina iliandika barua kwa ajili ya kuhoji matumizi hayo.

Akijibu swali hilo la nyongeza, Waziri wa fedha William Mgimwa alisema, swali lake kama linahusu 2010/211 tunalichukua na tutalifanyia kazi.

Katika swali lake la msingi, mbunge huyo alihoji kiasi kilichokusanywa wizara ya fedha katika halmashauri zote nchini, lakini pia alitaka kujua fedha hizo zilitumika kwa shughuli gani.

“Katika mwaka wa fedha 2010/11, Wizara ya Fedha kupitia barua yenye kumb. Na eb/40/01/vol.5/003, iliagiza jumla ya Sh milioni 175 za Kitanzania, zirejeshwe hazina kutoka katika halmashauri ya wilaya ya Kigoma, ufuatiliaji unaonyesha kuwa halmashauri zote nchini, ziliagizwa kurejesha fedha kwa mtindo huo.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri huyo alisema, Agosti 2011 ilibainika fedha za matumizi ya kawaida (OC) za mwezi zilizotumwa kwenye halmashauri, zilizidi kiasi kilichokuwa kimeidhinishwa na kikao cha Resources and Expenditure Celling Comité, ambapo jumla ya Sh bilioni 12, ziliizinishwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida kwenye halmashauri zote nchini.
Na Mtanzania

No comments:

Post a Comment