Pages


Photobucket

Sunday, November 18, 2012

HILI NDILO TAMKO LA CHADEMA DHIDI YA POLISI


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema ) kumetoa tamko kumtaka Rais Jakaya Kikwete kuonyesha dhamira ya kushughulikia malalamiko waliyotoa kwake dhidi ya matumizi ya polisi kupambana na wakosoaji wa CCM na serikali.

Tamko hilo limo kwenye taarifa ya Chadema iliyotolewa na Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama Wilfred Lwakatare, iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam.

Katika andiko hilo, walimtaka Rais Kikwete atekeleze mambo yaliyoandikwa kwenye barua ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, aliyetaka serikali ifanye uchunguzi wa matukio ya utesaji yaliyofanywa na vyombo vya dola dhidi ya wanaoipinga serikali.

Waraka huo ulitaka uchunguzi ufanyike dhidi ya polisi waliotumika kuteka, kutesa na kuua kwa malengo ya kisiasa ya kupambana na wakosoaji wa chama tawala na serikali yake.

Katika taarifa yake, Chadema ilisema walimwandikia Rais wakitaka kufanyike uchunguzi huru kwa kuunda Tume ya Kimahakama/Kijaji ili ukweli ujulikane na haki ionekane ikitendeka badala ya kutoa lugha ya kisiasa kwa nia ya kujikosha mbele ya umma, wakati CCM na polisi, wanakaa na kupanga mikakati inayopelekea kudhulumu haki na roho za Watanzania.

Aidha, wakati uchunguzi huo ukifanyika, watuhumiwa wote, wakiwemo viongozi wa CCM, serikali na watendaji wa Jeshi la Polisi waliokubali kutumika, hata kuvunja haki za binadamu, katiba na sheria, wanawajibika kwa wao kujiuzulu au kufukuzwa kazi.


Rwakatare alisema kauli iliyotolewa na Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete kuwataka viongozi na wanachama wa chama hicho waache kutegemea Jeshi la Polisi katika kukabiliana na wapinzani ni ushahidi wa tuhuma ambazo Chadema imekuwa ikitoa dhidi ya chama hicho.

Hivi karibuni Rais Kikwete, alikitahadharisha chama hicho kuwa kikitegemea zaidi polisi kwamba ndiyo msaada kwake katika kujibu mapigo ya wapinzani kitashindwa.

Akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Nane CCM baada ya kuchaguliwa kwa mara nyingine kuwa Mwenyekiti kwa miaka mingine mitano, alisema viongozi wa CCM lazima wajipange na kuwa wepesi wa kujibu mapigo ya wapinzani.

Alisema jawabu la siasa siyo polisi bali ni wanasiasa wenyewe na kwamba polisi hawawezi kuwa jibu la suala la siasa lazima kila kiongozi ajitambue yeye mwenyewe ndiyo mwenezi katika eneo lake.

Chadema ilisema Watanzania wanajua kuwa matukio ya vyombo vya dola kuhujumu wapinzani na wakosoaji wa serikali ya CCM, kwa nia ya kuilinda CCM, yamekwenda kwa sababu watu na makundi ya kijamii pia wameanza kuandamwa.

“Mtu, watu au makundi mbalimbali ya kijamii ambayo yanaonekana kutoa mawazo mbadala, kudai haki na uwajibikaji yameanza kuandamwa. Mifano mizuri hapa ni kufungiwa kwa Gazeti la Mwanahalisi na kutekwa na kuteswa kwa kiongozi wa madaktari, Dk. Steven Ulimboka. “ ilisema taarifa ya Rwakatare.

Chadema ilisema ukweli huo umesaidia kumaliza fumbo lililokuwepo juu ya madai ya muda mrefu kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa na viongozi wa CCM na watendaji wa serikali.

“Kauli hiyo ya Kikwete imetufikisha kwenye kilele cha ushahidi kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa kukabiliana na hoja na shughuli halali za kisiasa zinazofanywa na Chadema , chama mbadala kwa sasa kinacholenga kuiondoa CCM madarakani”.

Aidha imesaidia kufumbua fumbo la kwa nini Jeshi la Polisi Mkoani Iringa lilitumia nguvu kubwa kuingilia shughuli halalli za Chadema kufanya mikutano ya ndani, ikiwemo ufunguzi wa matawi katika Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa, na hatimaye kusababisha kifo cha Mwanandishi wa Habari, Daudi Mwangosi, Septemba mwaka huu.
 
chanzo : NIPASHE

No comments:

Post a Comment