Pages


Photobucket

Saturday, November 17, 2012

HOFU,VILIO VYAIGUBIKA KAGERA



na Victor Eliud (Tanzania Daima)

MAMIA ya wakazi wa vijiji vinne katika kata ya Kalambi, wilaya ya Muleba, mkoani Kagera, hawana mahali pa kuishi baada ya nyumba zao kuvunjwa chini ya Operesheni Okoa Mazingira iliyosimamiwa na vyombo vya dola likiwemo jeshi la polisi, usalama wa taifa na TAKUKURU.
Umati mkubwa wa watu, wakiwemo wanawake wajawazito na wenye watoto wachanga, uliangua vilio kuona nyumba zake zikichomwa moto na kubomolewa na askari hao kwa madai kuwa ni wahamiaji haramu huku wakiwa wameishi katika vijiji hivyo kwa miaka mingi.
Vijiji vilivyokumbwa na zahama hiyo, ni vya Bitunzi, Nyabilanda, Kasharara na Kyebitembe, ambapo sasa hawana mahali pa kuishi huku wengine wakiweka kambi kwenye nyumba za ibada.
Wakizungumza na Tanzania Daima Jumamosi, iliyotembelea eneo la tukio na kushuhudia uharibifu mkubwa uliofanywa katika operesheni hiyo, baadhi ya wanawake walidai kujifungua wakiwa hawana msaada wowote wala mahali pa kuishi na kwamba wamekuwa wakikesha na kulala chini ya miti na watoto wao.
Aidha wananchi hao waliwashutumu baadhi ya askari polisi kwa kupora pesa na mifugo yao kinyume cha sheria na baadhi ya wananchi waliopinga ukandamizaji huo, walikamatwa na kubambikiwa kesi.
Walidai kuwa polisi hao wamepora sh milioni 40 wakati wa operesheni hiyo na magunia 140 ya nafaka huku wakiwaacha wananchi hao wakiteseka kwa njaa.
Walisema mbali ya polisi hao waliokuwa na silaha za moto na mabomu ya machozi, pia walifyeka mazao yao na hata walipohoji walitishiwa kufungwa jela kwa vile wamevamia na kujenga maeneo yasiyoruhusiwa kisheria.
Imedaiwa kuwa zaidi ya nyumba zao 105 zimechomwa moto na polisi hao kwa siku moja tu ya Novemba mosi mwaka huu.
Siyengo Sanane, mkazi wa maeneo hayo, alisema kuwa jitihada zao za kuwaona viongozi wa wilaya zimekwama na wamekuwa wakitishwa ili wasidai haki zao.
“Unajua haya maeneo yetu yanataka kumilikishwa kwa Wanyarwanda wala siyo kweli kwamba sisi tumevamia na kujenga hapa…tumeishi hapa zaidi ya miaka 15 iweje leo ndiyo tuonekane wavamizi?
“Sijawahi kuona serikali isiyojali watu wake..hii ni danganya toto..sisi tuna taarifa kuwa hizi ni njama za kuwaleta wahamiaji haramu ili tukishaondolewa hapa, wao ndio wamilikishwe maeneo yetu nasi hatutakubali na lazima damu imwagike,” alisema.
Mwenyekiti wa kijiji cha Kyebitembe, Paschal Mnyangote, alikiri kupata fununu za kuwepo njama ya kutaifishwa kwa maeneo hayo ili wakabidhiwe wawekezaji na kuahidi kuwaamuru wananchi hao kupambana na wahamiaji hao na kuwataka wasikubali kuondoka kwenye maeneo hayo kwa kuwa ni unyanyaswaji na ni kinyume cha haki za binadamu.
“Ni kweli hizi taarifa zipo na hii ni danganya toto kwamba wamevamia hifadhi…nimewaahidi wananchi wangu iwapo serikali haitazinduka nitawaamuru wananchi wangu wawafanye watakavyo hawa Wanyarwanda maana sintokubali waonewe nami kama kiongozi wao ninaona,” alisema mwenyekiti.
Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Lembiris Kipuyo, alipohojiwa kwa njia ya simu alikiri nyumba za wananchi hao kuchomwa na kubomolewa na kuwa wamefanya hivyo, ili kulinda mazingira ya mkoa huo.
“Kuna operesheni okoa mazingira ya mkoa wa Kagera inaendelea kwenye wilaya tatu za Biharamlo, Kagera na Mleba kwenye mkoa wetu, ili kuwahamisha wahamiaji haramu wanaoingia na makundi makubwa ya ng’ombe katika misitu ya hifadhi.
“Ni operesheni ya wazi maana inaendeshwa na polisi na inasimamiwa na maafisa usalama wa taifa, TAKUKURU na wanasheria..hivyo wanaolalamika hawajui kwamba kuishi kwenye ardhi kinyume cha sheria ni kosa,” alisema Kivuyo.

No comments:

Post a Comment