MAMIA ya wakazi wa vijiji vinne katika kata ya Kalambi, wilaya 
ya Muleba, mkoani Kagera, hawana mahali pa kuishi baada ya nyumba zao 
kuvunjwa chini ya Operesheni Okoa Mazingira iliyosimamiwa na vyombo vya 
dola likiwemo jeshi la polisi, usalama wa taifa na TAKUKURU.
  Umati mkubwa wa watu, wakiwemo wanawake wajawazito na wenye watoto 
wachanga, uliangua vilio kuona nyumba zake zikichomwa moto na kubomolewa
 na askari hao kwa madai kuwa ni wahamiaji haramu huku wakiwa wameishi 
katika vijiji hivyo kwa miaka mingi.
  Vijiji vilivyokumbwa na zahama hiyo, ni vya Bitunzi, Nyabilanda, 
Kasharara na Kyebitembe, ambapo sasa hawana mahali pa kuishi huku 
wengine wakiweka kambi kwenye nyumba za ibada.
  Wakizungumza na Tanzania Daima Jumamosi, iliyotembelea eneo la tukio 
na kushuhudia uharibifu mkubwa uliofanywa katika operesheni hiyo, baadhi
 ya wanawake walidai kujifungua wakiwa hawana msaada wowote wala mahali 
pa kuishi na kwamba wamekuwa wakikesha na kulala chini ya miti na watoto
 wao.
  Aidha wananchi hao waliwashutumu baadhi ya askari polisi kwa kupora 
pesa na mifugo yao kinyume cha sheria na baadhi ya wananchi waliopinga 
ukandamizaji huo, walikamatwa na kubambikiwa kesi.
  Walidai kuwa polisi hao wamepora sh milioni 40 wakati wa operesheni 
hiyo na magunia 140 ya nafaka huku wakiwaacha wananchi hao wakiteseka 
kwa njaa.
  Walisema mbali ya polisi hao waliokuwa na silaha za moto na mabomu ya 
machozi, pia walifyeka mazao yao na hata walipohoji walitishiwa kufungwa
 jela kwa vile wamevamia na kujenga maeneo yasiyoruhusiwa kisheria.
  Imedaiwa kuwa zaidi ya nyumba zao 105 zimechomwa moto na polisi hao  kwa siku moja tu ya Novemba mosi mwaka huu.
  Siyengo Sanane, mkazi wa maeneo hayo,  alisema kuwa jitihada zao za 
kuwaona viongozi wa wilaya  zimekwama na wamekuwa wakitishwa ili wasidai
 haki zao.
  “Unajua haya maeneo yetu yanataka kumilikishwa kwa Wanyarwanda wala 
siyo kweli kwamba sisi tumevamia na kujenga hapa…tumeishi hapa zaidi ya 
miaka 15 iweje leo ndiyo tuonekane wavamizi?
  “Sijawahi kuona serikali isiyojali watu wake..hii ni danganya 
toto..sisi tuna taarifa kuwa hizi ni njama za kuwaleta wahamiaji haramu 
ili tukishaondolewa hapa, wao ndio wamilikishwe maeneo yetu nasi 
hatutakubali na lazima damu imwagike,” alisema.
  Mwenyekiti wa kijiji cha Kyebitembe, Paschal Mnyangote,  alikiri 
kupata fununu za kuwepo njama ya kutaifishwa kwa maeneo hayo ili 
wakabidhiwe wawekezaji na kuahidi kuwaamuru wananchi hao kupambana na 
wahamiaji hao na kuwataka wasikubali kuondoka kwenye maeneo hayo kwa 
kuwa ni unyanyaswaji na ni kinyume cha haki za binadamu.
  “Ni kweli hizi taarifa zipo na hii ni danganya toto kwamba wamevamia 
hifadhi…nimewaahidi wananchi wangu iwapo serikali haitazinduka 
nitawaamuru wananchi wangu wawafanye watakavyo hawa Wanyarwanda maana 
sintokubali waonewe nami kama kiongozi wao ninaona,” alisema mwenyekiti.
  Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Lembiris Kipuyo, alipohojiwa kwa njia ya 
simu alikiri nyumba za wananchi hao kuchomwa na kubomolewa na kuwa 
wamefanya hivyo, ili kulinda mazingira ya mkoa huo.
  “Kuna operesheni okoa mazingira ya mkoa wa Kagera inaendelea kwenye 
wilaya tatu za Biharamlo, Kagera na Mleba kwenye mkoa wetu, ili 
kuwahamisha wahamiaji haramu wanaoingia na makundi makubwa ya ng’ombe 
katika misitu ya hifadhi.
  “Ni operesheni ya wazi maana inaendeshwa na polisi na inasimamiwa na 
maafisa usalama wa taifa, TAKUKURU na wanasheria..hivyo wanaolalamika 
hawajui kwamba kuishi kwenye ardhi kinyume cha sheria ni kosa,” alisema 
Kivuyo.
 
No comments:
Post a Comment