Na Rajab Ramah, Nairobi
Wasiwasi unaongezeka juu ya uwezo wa vikosi vya usalama vya Kenya 
kuzuwia vurugu na kujibu matatizo kwa ufanisi huku uchaguzi mkuu ukiwa 
umebakia miezi mitatu tu, vikundi vya asasi za kiraia vyasema.

Afisa
 wa Kitengo cha Huduma Maalumu akimpiga teke kijana wa kenya katika 
kitongoji cha Eastleigh Nairobi hapo tarehe 19 Novemba, siku moja baada 
ya bomu kulipuka katika basi dogo, lililowaua watu saba. [Na Carl de 
Souza/AFP]
Tabia za polisi hivi karibuni katika kukabiliana na vitisho vya usalama 
zimezua hofu na wasiwasi kuliko uhakika miongoni mwa wananchi, kwa 
mujibu wa Odhiambo Oyoko, mratibu mtendaji wa Kituo cha Uimarishaji Haki
 na Ulinzi.
"Kila operesheni ya polisi katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu 
huishia katika kukamata watu kwa makundi bila ya kuchagua, ubakaji, 
uvamizi, au aina nyengine ya vurugu [zinazoelekezwa] kwa watu wasio na 
hatia. Hili ni kinyume na dhamiri ya kupambana na uhalifu," alisema, 
akikisudia operesheni za karibuni huko Tana River Delta, Baragoi, 
Eastleigh na Garissa.
Mwezi wa Septemba, zaidi ya watu 100 waliuawa katika mapambano ya 
kikabila huko Tana River Delta, wakiwemo maafisa wa polisi tisa, kabla 
ya vikosi vya usalama kuweza kuidhibiti hali hiyo.
Tarehe 10 Novemba, polisi 42 waliuawa na majambazi huko Baragoi Wilaya 
ya Samburu katika Mkoa wa Bonde la Ufa. Kutokana na madai kuwa polisi 
walichukua hatua kwa taratibu katika kushughulikia mzozo huo, Rais wa 
Kenya Mwai Kibaki alipeleka Vikosi vya Ulinzi vya Kenya katika eneo hilo
 ili kuwasaidia polisi.
Siku tisa baadaye, kuuliwa kwa risasi askari watatu wa Vikosi vya Ulinzi
 vya Kenya huko Garissa kulipelekea maafisa wa jeshi kulipiza kisasi kwa
 jamii katika ghasia za utumiaji nguvu.
Kukosekana na uratibu, polisi wenye zana hafifu
Simiyu Werunga, mkurugenzi wa Kituo cha Afrika cha Masomo ya Usalama na 
Mikakati kilichoko Nairobi, alisema kuwa hadithi kama hizo zimekuwa za 
kawaida sana katika miezi ya karibuni, na mara nyingi mashambulizi ya 
kigaidi ndio huifanya hali kuwa mbaya zaidi.
Werunga, kapteni wa jeshi mstaafu, alisema kukosekana kwa uratibu 
miongoni mwa vyombo vya usalama ndio sababu ya kuendelea kukosekana kwa 
usalama.
"Tumeona kesi ambapo jeshi au Kitengo cha Huduma Maalumu kinapelekwa ili
 kushughulikia kutokuwepo kwa usalama, ambapo polisi wa kawaida 
wangeweza kuidhibiti hali hiyo," aliiambia Sabahi. "Hali hii unazua 
mtafaruku na kuleta hofu kwa umma."
Alisema kuwa hatua madhubuti za usalama zinapasa kuchukuliwa mara moja 
ili kuwahakikishia Wakenya uchaguzi wa amani na salama hapo tarehe 4 
Machi 2013.
"Kuna haja ya kuwa na mkabala ulioratibiwa vyema ambao utavijumuisha 
vyombo vyote katika kugundua na kushughulikia uhalifu," alisema. "Hii 
inaweza kutokea iwapo vitengo vyote vya polisi vimewekwa chini ya 
uongozi mmoja wa mkoa."
Polisi wanapaswa kuacha kutoa adhabu za kubambikiza kwa wenyeji wa 
maeneo ya uhalifu, alisema. Badala yake, wanatakiwa wajenge mahusiano na
 jamii ambazo badala yake zinasaidia kutoa intelijensia yenye thamani 
ambayo itapelekea kukamatwa kwa wahalifu.
Alisema kuwa ghasia za karibuni za askari huko Garissa na operesheni 
zisizochagua zinazowalenga watu wa jamii ya Wasomali katika kitongoji 
cha Eistleigh huko Nairobi kumemomonyoa mafungamano na uaminifu baina ya
 polisi na jamii.
Philip Onguje, mratibu wa Jukwaa la Mageuzi ya Usalama, kikundi cha 
kijamii ambacho kinatetea mageuzi ya sekta ya usalama nchini Kenya, 
aliiambia Sabahi kuwa polisi wana zana hafifu za kuweza kushughulikia 
miendo inayoibuka ya uhalifu.
Alisema iko haja ya kuwafunza upya polisi katika kudhbiti mizozo ya 
uchaguzi na udhibiti wa makundi ili kuepuka matumizi ya nguvu kupita 
kiasi au operesheni za usalama zinazopendelea au kuonea upande mmoja.
Onguje alisema kuwa utafiti uliofanywa na jumuiya yake mwezi uliopita 
zilionesha kuwa hakuna hata kituo kimoja cha polisi nchini kati ya vituo
 456 kina vifaa vya usalama au uwezo wa kupambana na uhalifu.
"Lilipaswa kuwa suala la kumshughulisha kila Mkenya," alisema. "Lazima 
sote tushinikize kwa kuwepo kwa marekebisho, kuvipatia vituo vya polisi 
vifaa na kuajiri maafisa wengi zaidi wa polisi ndani ya miezi michache 
iliyobakia ili waweze kuhakikisha uchaguzi wa salama mwaka ujao."
Serikali inashughulikia kasoro
Kaimu Katibu Mkuu wa Usalama wa Ndani Mutea Iringo aliiambia Sabahi kuwa
 serikali inashughulikia wasiwasi huu na inao udhibiti wa usalama wa 
nchi.
Alisema kuwa serikali inakusudia kuwapa mafunzo maafisa polisi 7,000 
ambao watapelekwa nchini kote ifikapo mwezi Januari ili kuliongezea 
nguvu jeshi la polisi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2013.
"Pia tutawapa mafunzo maafisa wote kwa uchaguzi, haki za binadamu na 
masuala mengine ya kipolisi na tunawahakikishia Wakenya kuwa katika 
uchaguzi ujao tutalindwa vyema na maafisa wetu," Iringo alisema.
Serikali pia imo katika mchakato wa kumajiri Inspekta Jenerali wa polisi
 katika juhudi za kuhamisha uongozi na kusaidia kupanga upya jeshi zima 
ili liweze kukabiliana na uhalifu kwa ufanisi, alisema.
Chanzo http://sabahionline.com
 
 

No comments:
Post a Comment