Pages


Photobucket

Friday, November 30, 2012

VIKOSI VYA USALAMA NCHINI KENYA VYAZUA TAFRANI KUELEKEA UCHAGUZI MKUU


Na Rajab Ramah, Nairobi
Wasiwasi unaongezeka juu ya uwezo wa vikosi vya usalama vya Kenya kuzuwia vurugu na kujibu matatizo kwa ufanisi huku uchaguzi mkuu ukiwa umebakia miezi mitatu tu, vikundi vya asasi za kiraia vyasema.

Afisa wa Kitengo cha Huduma Maalumu akimpiga teke kijana wa kenya katika kitongoji cha Eastleigh Nairobi hapo tarehe 19 Novemba, siku moja baada ya bomu kulipuka katika basi dogo, lililowaua watu saba. [Na Carl de Souza/AFP]

Tabia za polisi hivi karibuni katika kukabiliana na vitisho vya usalama zimezua hofu na wasiwasi kuliko uhakika miongoni mwa wananchi, kwa mujibu wa Odhiambo Oyoko, mratibu mtendaji wa Kituo cha Uimarishaji Haki na Ulinzi.

"Kila operesheni ya polisi katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu huishia katika kukamata watu kwa makundi bila ya kuchagua, ubakaji, uvamizi, au aina nyengine ya vurugu [zinazoelekezwa] kwa watu wasio na hatia. Hili ni kinyume na dhamiri ya kupambana na uhalifu," alisema, akikisudia operesheni za karibuni huko Tana River Delta, Baragoi, Eastleigh na Garissa.

Mwezi wa Septemba, zaidi ya watu 100 waliuawa katika mapambano ya kikabila huko Tana River Delta, wakiwemo maafisa wa polisi tisa, kabla ya vikosi vya usalama kuweza kuidhibiti hali hiyo.

Tarehe 10 Novemba, polisi 42 waliuawa na majambazi huko Baragoi Wilaya ya Samburu katika Mkoa wa Bonde la Ufa. Kutokana na madai kuwa polisi walichukua hatua kwa taratibu katika kushughulikia mzozo huo, Rais wa Kenya Mwai Kibaki alipeleka Vikosi vya Ulinzi vya Kenya katika eneo hilo ili kuwasaidia polisi.

Siku tisa baadaye, kuuliwa kwa risasi askari watatu wa Vikosi vya Ulinzi vya Kenya huko Garissa kulipelekea maafisa wa jeshi kulipiza kisasi kwa jamii katika ghasia za utumiaji nguvu.

Kukosekana na uratibu, polisi wenye zana hafifu

Simiyu Werunga, mkurugenzi wa Kituo cha Afrika cha Masomo ya Usalama na Mikakati kilichoko Nairobi, alisema kuwa hadithi kama hizo zimekuwa za kawaida sana katika miezi ya karibuni, na mara nyingi mashambulizi ya kigaidi ndio huifanya hali kuwa mbaya zaidi.

Werunga, kapteni wa jeshi mstaafu, alisema kukosekana kwa uratibu miongoni mwa vyombo vya usalama ndio sababu ya kuendelea kukosekana kwa usalama.

"Tumeona kesi ambapo jeshi au Kitengo cha Huduma Maalumu kinapelekwa ili kushughulikia kutokuwepo kwa usalama, ambapo polisi wa kawaida wangeweza kuidhibiti hali hiyo," aliiambia Sabahi. "Hali hii unazua mtafaruku na kuleta hofu kwa umma."

Alisema kuwa hatua madhubuti za usalama zinapasa kuchukuliwa mara moja ili kuwahakikishia Wakenya uchaguzi wa amani na salama hapo tarehe 4 Machi 2013.

"Kuna haja ya kuwa na mkabala ulioratibiwa vyema ambao utavijumuisha vyombo vyote katika kugundua na kushughulikia uhalifu," alisema. "Hii inaweza kutokea iwapo vitengo vyote vya polisi vimewekwa chini ya uongozi mmoja wa mkoa."

Polisi wanapaswa kuacha kutoa adhabu za kubambikiza kwa wenyeji wa maeneo ya uhalifu, alisema. Badala yake, wanatakiwa wajenge mahusiano na jamii ambazo badala yake zinasaidia kutoa intelijensia yenye thamani ambayo itapelekea kukamatwa kwa wahalifu.

Alisema kuwa ghasia za karibuni za askari huko Garissa na operesheni zisizochagua zinazowalenga watu wa jamii ya Wasomali katika kitongoji cha Eistleigh huko Nairobi kumemomonyoa mafungamano na uaminifu baina ya polisi na jamii.

Philip Onguje, mratibu wa Jukwaa la Mageuzi ya Usalama, kikundi cha kijamii ambacho kinatetea mageuzi ya sekta ya usalama nchini Kenya, aliiambia Sabahi kuwa polisi wana zana hafifu za kuweza kushughulikia miendo inayoibuka ya uhalifu.

Alisema iko haja ya kuwafunza upya polisi katika kudhbiti mizozo ya uchaguzi na udhibiti wa makundi ili kuepuka matumizi ya nguvu kupita kiasi au operesheni za usalama zinazopendelea au kuonea upande mmoja.

Onguje alisema kuwa utafiti uliofanywa na jumuiya yake mwezi uliopita zilionesha kuwa hakuna hata kituo kimoja cha polisi nchini kati ya vituo 456 kina vifaa vya usalama au uwezo wa kupambana na uhalifu.

"Lilipaswa kuwa suala la kumshughulisha kila Mkenya," alisema. "Lazima sote tushinikize kwa kuwepo kwa marekebisho, kuvipatia vituo vya polisi vifaa na kuajiri maafisa wengi zaidi wa polisi ndani ya miezi michache iliyobakia ili waweze kuhakikisha uchaguzi wa salama mwaka ujao."

Serikali inashughulikia kasoro
Kaimu Katibu Mkuu wa Usalama wa Ndani Mutea Iringo aliiambia Sabahi kuwa serikali inashughulikia wasiwasi huu na inao udhibiti wa usalama wa nchi.

Alisema kuwa serikali inakusudia kuwapa mafunzo maafisa polisi 7,000 ambao watapelekwa nchini kote ifikapo mwezi Januari ili kuliongezea nguvu jeshi la polisi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2013.

"Pia tutawapa mafunzo maafisa wote kwa uchaguzi, haki za binadamu na masuala mengine ya kipolisi na tunawahakikishia Wakenya kuwa katika uchaguzi ujao tutalindwa vyema na maafisa wetu," Iringo alisema.

Serikali pia imo katika mchakato wa kumajiri Inspekta Jenerali wa polisi katika juhudi za kuhamisha uongozi na kusaidia kupanga upya jeshi zima ili liweze kukabiliana na uhalifu kwa ufanisi, alisema.

No comments:

Post a Comment