WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na mtoto wa Rais Jakaya Kikwete, 
Ridhiwan wamezungumzia tuhuma ambazo zimekuwa zikielekezwa kwao kwamba 
wanamiliki rasilimali zenye thamani ya mabilioni ya shilingi.

Ridhiwan Kikwete 
Lowassa kwa upande wake amekuwa akidaiwa kuwa tajiri anayemiliki kampuni
 kubwa za kibiashara na kumekuwa na taarifa kwamba ana ukwasi ambao 
vyanzo vyake vinatia shaka na siyo rahisi kuvitolea maelezo.
Kwa upande wake Ridhiwan naye amekuwa akidaiwa kuwa na utajiri mkubwa na
 amekuwa akihusishwa na biashara za kampuni za kusafirisha mafuta ambayo
 hupelekwa kwenye migodi, umiliki wa hoteli na majengo kadhaa ya 
kifahari.
Wote wawili wamekuwa wakidaiwa kwamba baadhi ya mali zao wamekuwa 
wakiziendesha chini ya kivuli cha wafanyabiashara wengine wakubwa nchini
 ili kukwepa kuhojiwa walikotoa utajiri huo, taarifa ambazo hata hivyo 
imekuwa vigumu kuzithibitisha.
Hata hivyo jana kwa nyakati na mazingira tofauti, Lowassa na Ridhiwan 
walijitokeza hadharani na kukanusha madai kwamba wao ni matajiri wa 
kupindukia.
Lowassa kwa upande wake akiwa mjini Mbeya alisema yeye siyo tajiri kama 
ambavyo imekuwa ikidaiwa lakini wakati huohuo akasema “sijafilisika”.
“Wengi wanasema kuwa mimi ni tajiri siyo kweli, lakini sijafilisika 
kutokana na kuchangia makanisa kwani nina marafiki wengi ambao 
wananisaidia katika kuchangia makanisa nao pia hawajafilisika,”alisema 
Lowassa.
Lowasa alitoa kauli hiyo alipokuwa akiendesha harambee ya kuchangia 
ujenzi wa hosteli ya wanachuo wanawake ambao ni wanafunzi wa Chuo Kikuu 
cha Theofilo Kisanji cha mkoani Mbeya, kinachomilikiwa na Kanisa la 
Moraviani Tanzania, Jimbo la Kusini Magharibi.
Kiongozi huyo ambaye alichangia kaisi cha Sh25 milioni, alisema kila mtu
 ana wajibu wa kuchangia elimu na kwamba mwanamke anapaswa kutazamwa kwa
 karibu zaidi kwani ndiye anayebeba jukumu kubwa la kutunza familia.
Kwa upande wake Ridhiwan alisema: “Ikiwa mimi ni tajiri wa kiasi 
kinachosemwa, basi mimi ninamzidi Bakhressa (Said Salim, mfanyabiashara 
maarufu Afrika Mashariki), maana nimepewa kila hoteli hapa mjini, 
kampuni za mafuta na kila biashara kubwa inayoanzishwa hapa mjini ni ya 
Ridhiwan”.
Said Salim Bakhressa ni mfanyabiashara ambaye anatajwa kuwa tajiri 
kuliko wote nchini na anashika nafasi ya pili katika nchi za Afrika 
Mashariki na Kati, huku akiwa miongoni mwa wafanyabiashara 10 
wanaonyemelea kuingia katika nafasi za juu za utajiri Afrika.
Hata hivyo Ridhiwan ambaye hivi karibuni alichaguliwa kuwa Mjumbe wa 
Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), aliongeza: “Ninaweza kuwa nafanya
 biashara moja au mbili, lakini siwezi kuwa mmiliki kiasi chote hicho 
cha mali.
Mtoto huyo wa Rais Kikwete alikuwa akijibu tuhuma kwamba magari yake 
kumi ya kusafirisha mafuta yamekamatwa na kuzuiwa katika mpaka wa Kenya 
na Tanzania, Namanga mkoani Arusha kutokana na kukwepa kodi, taarifa 
ambayo aliikanusha.
 
 

No comments:
Post a Comment