Pages


Photobucket

Thursday, December 27, 2012

Wazazi hospitali kubwa walala ‘mzungu wa nne’ wodini


HALI si shwari kwenye wodi za wazazi katika hospitali karibu zote kubwa nchini baada ya kubainika kuwa wagonjwa wanalala kati ya wawili na watatu (maarufu kama mzungu wa nne), kwenye kitanda kimoja na wengine sakafuni wakisubiri kujifungua.

Wakimama wakiwa wamelala zaidi ya mmoja kwenye kitanda katika hospitali ya Amana jijini Dar es Salaam.Picha na Maktaba

Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi katika baadhi ya hospitali za rufaa na baadhi ya hospitali za mikoa, umebaini kuwa kama hali hiyo haitashughulikiwa haraka, kuna hatari ya wazazi hao na vichanga vyao, kuambukizana magonjwa.

Hospitali hizo ni Muhimbili, KCMC (Moshi), Bombo (Tanga), Hospitali za Mikoa ya Morogoro, Dodoma, Mwananyamala, Temeke na Amana za Dar es Salaam.

Hospitali zilizopo Dar es Salaam

Mgonjwa Zawadi Salehe aliyelazwa Wodi namba 38 Muhimbili, alisema siku ya kwanza alilazwa kwenye kitanda kilichokuwa na mgonjwa mwingine na baada ya kujifungua kwa upasuaji, alitakiwa kulala sakafuni ili kupisha kitanda kitumiwe na wagonjwa wengine.

“Ukifika (wodini) unapelekwa kwenye kitanda ambacho tayari kina mgonjwa. Inapofika siku ya Jumanne na Jumapili wanaletwa wagonjwa wengi zaidi ambao wamepewa rufaa ya kuja hapa. Wakishaingia, sisi ambao tulikuwapo tunaambiwa na wauguzi tulale chini ambako godoro moja wanalala watu watatu na wanaokosa nafasi kwenye godoro wanatandika kanga zao na kulala sakafuni.”

Ofisa Habari wa Hospitali hiyo, Aminieli Aligaesha alikiri kuwapo kwa tatizo hilo na kueleza kuwa inatokana na uhaba wa nafasi wodini na siyo vitanda. Alisema Muhimbili inapokea zaidi ya wagonjwa 70 kila wodi.

“Kila wodi ina vitanda 26. Wagonjwa wanapozidi huwezi kuwarudisha nyumbani. Kutokana na ukosefu wa vitanda hulazimika kuwalaza chini kwenye magodoro huku tiba ikiendelea.”

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Amana, Dk Meshack Shimwela alisema kwamba wodi ya wazazi katika hospitali hiyo inapokea wagonjwa wengi, lakini wengi wao hawana matatizo makubwa na walipaswa kwenda katika vituo vya afya.

“Hii ni Hospitali ya Rufaa, tunapokea wagonjwa wenye matatizo makubwa tu hivyo wagonjwa wanaojifungua kwa njia ya kawaida wanatakiwa waende katika vituo vya afya vilivyopo katika maeneo yao, lakini utakuta kila mgonjwa anakimbilia hapa ndiyo maana kuna huu msongamano wa mkubwa,” alisema Dk Shimwela.

Katika Hospitali ya Mwananyamala, mgonjwa Elizabeth Mgimwa alisema: “Kwenye wodi hii ya wazazi kinachoangaliwa ni hela, kama hauna huyo mzazi atatukanwa na nesi na hata huduma muhimu hatapatiwa kwa wakati.”

Katibu wa Afya katika Hospitali hiyo, Edwin Bisakala alikiri kupata taarifa za baadhi ya wagonjwa kutoa fedha kwa wauguzi lakini akaeleza kuwa malipo hayo hutolewa kama asante. Hata hivyo alisema: “Tunataka mama ambaye ameombwa fedha atoe ushirikiano kwenye uongozi wa hospitali kwa kuwa haitakiwi mgonjwa kutoa asante. Hawa wauguzi wameajiriwa kwa kazi hiyo.”

Hospitali ya Mkoa Dodoma

Wajawazito katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma wanalalamikia kile wanachokiita manyanyaso kutoka kwa wauguzi wa wodi ya wazazi, huku baadhi wakielezea kitendo cha kulazwa sakafuni kuwa ni kero.Akizungumzia malalamiko hayo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Ezekiel Mpuya alisema uongozi una tabia ya kuwaita wauguzi wanaolalamikiwa na wagonjwa kisha kuwaonya.

“Kwa sasa malalamiko ya kunyanyaswa wajawazito kwa kiasi kikubwa yamepungua baada ya uongozi kuanza kumshughulikia mtu mmoja baada ya mwingine,” alisema.

Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment