Pages


Photobucket

Saturday, September 14, 2013

Mwakyembe: Ujenzi wa bandari ya Mwambani kuanza Desemba

Serikali imesisitiza kuanza rasmi ujenzi wa Bandari ya Mwambani katika kipindi cha miezi mitatu ijayo hatua ambayo itaenda sambamba na uunganishwaji wa reli kutoka Tanga-Arusha mpaka Musoma. Hayo yalibainishwa jana na Waziri wa Uchukuzi Dk.Harrison Mwakyembe wakati wa kikao cha wadau wa sekta ya uchukuzi mkoa wa Tanga kilichofanyika jijini hapa. Dk.Mwakyembe alisema kimsingi serikali imeshakamilisha zoezi la ulipaji fidia katika eneo hilo ambapo zaidi ya shilingi bilioni 6 zililipwa kwa wananchi ili kupisha ujenzi wa Bandari hiyo na kwamba makampuni 22 yamejitokeza kwa ajili ya uwekezaji kwenye eneo hilo.

“Upembuzi yakinifu ulishafanyika na tafiti mbalimbali zilishafanyika kwa ajili ya kuangalia mahusiana ya bandari na reli sasa kilichobaki ni kuanza ujenzi na na upembuzi yakinifu na kwamba tayari makampuni 22 na 12 yamekuwa short listed,”alisema.
Hata hivyo, aliutaka uongozi wa mkoa wa Tanga kuhakikisha unatumia fursa ya Jukwaa la uwekezaji Kanda ya Kaskazini linalitarajiwa kufanyika Septemba 26 na 27 mwaka huu katika kufungua fursa za uwekezaji kwenye sekta mbalimbali ikiwemo miundo mbinu ya reli na Anga.
Aidha aliiagiza Kampuni hodhi ya Rasilimali za Reli( RAHCO) kufanya ukarabati wa njia ya reli katika eneo la Mombo-Mkomazi mpaka Taveta ilikurahisisha usafairishaji wa mizigo unaofanyika katika njia hiyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Huduma za Ushirika wa Kampuni hodhi ya Rasilimali za Reli( RAHCO) Mbuttolwe Kabeta alisema kuwa mpango wa ujenzi wa Reli kutoka Mwambani-Arusha mpaka Musoma upo katika mkakati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki(EAC) na kwamba tafiti mbalimbali zilishafanyika kwa ajili ya mchakato huo.
Kabeta alisema kwa sasa Washauri elekezi kwa ajili ya usanifu,utafuti na upembuzi yakinifu wameshapatikana kutoka nchini Ujerumani na kwamba shilingi bilioni 5.2 zimetengwa kwa ajili ya usanifu na utafiti na shilingi bilioni 4.9 zimetengwa kwa ajili ya kulipa fidia.
“Mradi wote kwa ajili ya shughuli mbalimbali unatarajiwa kutumia zaidi ya shilingi bilioni 15.5 na kwa upande wa fidia mpaka sasa bilioni 4.6 zimeshalipwa hivyo tayari tumeanza mchakato wa utekelezaji wa mradi huo”,alisisitiza Mkurugenzi huyo. 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment