Pages


Photobucket

Saturday, September 14, 2013

Mbinu mpya za kusafirisha dawa za kulevya zabainika

Wakati vyombo vya sheria vikiendelea kupambana na biashara ya dawa za kulevya nchini, wasafirishaji hao kila siku wanaendelea kuwa wabunifu na kubuni mbinu mpya na za kutisha za kusafirisha dawa hizo kutoka eneo moja hadi lingine. Imebainika kuwa miongoni mwa mbinu mpya wanazotumia ni kusafirisha dawa hizo kwa kutumia ndege za mizigo ambapo huweza kuweka dawa za kulevya kwenye mdoli, jarida, makopo ya maziwa ya watoto, vinyago vya kimakonde na kuutuma kama kifurushi kwenda sehemu nyingine.
Pia, wasafirishaji hao kwa sasa wanaweza kuvaa kama watawa (masista na mapadre) na kujifanya wameshika rozari zao wakisali na kumbe wamehifadhi dawa hizo ndani ya mavazi yao makubwa.
Pia, imebainika kuwa siku hizi si lazima kusafirisha dawa za kulevya zilizo tayari bali kemikali zinazotumika kutengeneza dawa za kulevya(kwa mfano amphetamine inayoweza kutengenezwa maabara), husafirishwa na baada ya kufika kemikali huchanganywa katika maabara za siri na dawa za kulevya huanza kusambazwa mitaani.
Kamishna Mkuu wa Polisi Kitengo cha Dawa za Kulevya, Alfred Nzowa alisema wasafirishaji hao wanabuni mbinu mpya kila kukicha lakini alitaja mbinu kuu ya kusafirisha mzigo mkubwa ni kwa njia ya meli au ndege za kukodi, za abiria au binafsi kupeleka mzigo kutoka nchi moja hadi nyingine.
“Dawa nyingi zinazosambazwa hapa zinakuja kwa njia ya meli. Zinapofika kwenye mipaka ya bahari ya nchi za Afrika Mashariki kama Mombasa na Dar es Salaam hupakuliwa na kuwekwa katika boti ndogo ndogo ziendazo kwa kasi na kusambazwa,” alisema Kamishna Nzowa.
Kwa mfano, ripoti ya mwaka 2013 ya Umoja wa Mataifa kitengo cha Uhalifu na Dawa za Kulevya (UNODC) inaeleza kuwa kwa sasa njia inayotumika kupitisha dawa za kulevya kufika Tanzania ni maeneo ya visiwani hasa Tanga na Zanzibar, ambapo wasafirishaji hutumia boti binafsi ndogo. Mzigo unaposhushwa hapa hupelekwa kama mizigo midogo midogo Dar es Salaam.
Nzowa alisema mbinu nyingine iliyobuniwa na inayotumiwa na wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya ni kusafirisha kwa kutumia ndege ndogo binafsi, ambazo huweza kupita bila kukaguliwa.
Nzowa alisema wasafirishaji hao wanaendelea kubuni mbinu nyingi kila siku ili kuwazidi ujanja wakaguzi walio katika viwanja vya ndege na katika mipaka, ambapo kwa sasa wasafirishaji wadogo wanaweza kuzificha katika soli za viatu, sehemu za siri au katika matiti.
“Tuliwahi kumkamata msichana mmoja wa Kifilipino ambaye kwa wakati mmoja alitumia mbinu tatu kuficha dawa aina ya heroin. Aliweka gramu 400 katika viatu, ambapo gramu 200 kiatu kimoja na gramu 200 katika kiatu cha kushoto. Alificha kiasi kingine kwenye matiti na kiasi kingine sehemu za siri,” alisema Nzowa.
Nzowa alisema wasafirishaji hao wanaendelea kubuni njia mpya kila siku, ambapo kwa sasa wamejikita zaidi kusafirisha kwa njia ya meli na ndege ili kuweza kusafirisha kiasi kikubwa bila kugundulika.
“Wale wasafirishaji wa ndani ya nchi wanatumia njia kama hizo za kumeza, lakini wale manguli wanatumia meli za kukodi na ndege binafsi. Wanaweza kusafirisha hata kilo 800 kwa wakati mmoja,” alisema Nzowa.
Msemaji wa Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya nchini Florence Mlay, alisema wasafirishaji hao kwa sasa wanatumia meli binafsi kusafirisha dawa hizo na baada ya kufika Tanzania zinashushwa katika bandari ndogo ndogo ikiwamo Oysterbay.
Mlay alisema kutokana na watuhumiwa wanaokamatwa Tume hiyo imegundua mbinu nzito zinazotumika kusafirisha dawa za kulevya, kwa mfano kuweka dawa za kulevya katika chupa za poda, biblia au majani ya chai.
“Wanaweka poda, katikati unga, kisha poda juu, ni vigumu kubainika. Lakini wengine wanatumia ma ‘hotpot’ ya vyakula kuzisindika dawa hizo” alisema Mlay.
Tume hiyo imegundua mbinu nyingine kama ya kutumia biblia ambapo wanachana karatasi katikati ya biblia kisha wanazifunga dawa kwa utaalamu mkubwa kiasi cha ‘scanner’ kutoweza kuzibaini.
Karatasi maalumu
Mlay alisema wasafirishaji wanatumia mbinu ya kuifunga mizigo hiyo kwa kutumia karatasi maalumu, ambayo huzuia mashine ya kukagulia mizigo kubaini utofauti wa mzigo huo na dawa za kulevya.
Kwa mfano bangi huweza kufungwa katika pakiti za majani ya chai na kufungwa kwa karatasi hiyo bila ‘scanner’ kugundua.
Chanzo kimoja cha habari ambacho kiliwahi kuwa mfanyabiashara mkubwa wa dawa za kulevya na mtumiaji, alizungumza na Mwananchi na kusema kuwa njia nyingine ya kushangaza inayotumiwa na wasafirishaji hao ni kuwatumia watoto wadogo ambao bila kufahamu hubebeshwa dawa hizo na kupita uwanja wa ndege au mipakani bila kukaguliwa.
“Dawa zinafungwa vizuri, zinawekwa katika begi la mgongoni la mtoto, kisha dawa zinapuliziwa marashi ili kuficha harufu. Si rahisi watoto kuhisiwa kuwa wamebeba dawa hizo,” kilisema chanzo chetu.
Alieleza mbinu nyingine kuwa wanaposafirisha dawa hizo kwa njia ya ndege za mizigo huweza kufunga boksi lenye dawa hizo kisha nje kuandika ni chakula cha mbwa, vitabu, matunda au mboga za majani na kumbe ndani kuna dawa hizo. Imebainika kuwa wakati mwingine wasafirishaji huweza kushonea dawa za kulevya katika ngozi ya mnyama, kisha kuificha na mbwa wa uwanja wa ndege wasiweza kubaini.
Chanzo hicho kilitaja mbinu kama kuficha dawa katika soli za viatu, katika chupa za maziwa ya watoto, au kuzisafirisha kwa kutumia mtu ambaye hajui alichobeba ni nini lakini watumaji wanakuwa wameufunga kwa ujanja.
Wasafirishaji hao inaelezwa kuwa wakati mwingine wanatumia magamba ya konono wa baharini kusweka dawa hizo, kisha huziba kwa gundi na kuweka katika mizigo yao na kuipitisha mipakani.
Ripoti ya UNODC inaeleza kuwa kwa mwaka 2012 pekee, Watanzania zaidi ya 400 walikamatwa kwa kujaribu kusafirisha kilo 260 za heroin na kilo 151 za cocaine.
Hivi karibuni watanzania wawili walikamatwa nchini Ethiopia wakisafirisha dawa za kulevya huku meli ya Tanzania ya Mv Gold Star ilikamatwa na tani 30 za bangi.
Pia Julai mwaka huu wasichana wawili wa kitanzania walikamatwa uwanja wa ndege wa OR Tambo wakiwa na mzigo mkubwa wa dawa za kulevya aina ya methamphetamine (Tik).

No comments:

Post a Comment