Pages


Photobucket

Friday, January 4, 2013

Zitto: Serikali inaweweseka


ASEMA KAULI ZA WAZIRI MUHONGO NI HATARI
NAIBU Katibu Mkuu wa Chadena, Kabwe Zitto, na wenyeviti wa vyama vya CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, na James Mbatia wa NCCR-Mageuzi, wameishukia serikali wakisema inaweweseka kutokana na kauli ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kukinzana na mkakati wa serikali.
Hatua hiyo inakuja siku moja tangu Waziri Muhongo akutane na waandishi na kuwakejeli wananchi wa mikoa ya kusini hususan Mtwara kuwa hawakupaswa kuandamana kupinga mpango wa serikali kusafirisha gesi kutoka huko kwenda Dar es Salaam kwa kuwa rasilimali ni za Watanzania wote.
Waziri Muhongo alidai kuwa wananchi wa Mtwara wanashawishiwa na wanasiasa ili kufanya vurugu ilhali gesi nyingi haiko kwao bali iko kwenye mipaka ya nchi baharini kwenye kina kirefu na kuongeza kuwa hata wao wamekuwa wakinufaika na rasilimali za mikoa mengine.
Katika taarifa yake, Zitto alisema kuwa mkuu wa mkoa wa Mtwara aliwaita Watanzania wa mkoa huo wahaini, wapuuzi na watu hatari huku Rais wa Jakaya Kikwete naye akiingia kwenye mjadala huo kwa kuonya watu wanaowaunga mkono wawanachi hao akiwaita watafuta umaarufu wa kisiasa na wanataka kuigawa nchi.
“Siku moja baada ya hotuba ya Rais, Waziri Muhongo alifanya mkutano na waandishi wa habari kueleza suala lilelile ambalo bosi wake alilielezea usiku wa kuamkia Mwaka Mpya 2013. Hii ni dalili ya serikali kuweweseka,” alisema.
Alisema kuwa katika kauli ya serikali, ambayo haikuwa na jipya zaidi ya wimbo uleule wa ‘kugawa nchi’ ‘umaarufu wa kisiasa’ serikali ilitaka kuonyesha umma kuwa watu wa Mtwara hawana shukurani.

Kwamba miaka yote toka Uhuru watu wa Mtwara wamekuwa wakilishwa na pamba, kahawa, chai, tumbaku na sukari na hivyo watu wa Mtwara na Lindi hawakuchangia hata kidogo kwenye hazina ya taifa.
“Hivyo wao kupigia kelele gesi yao ni uchoyo na roho mbaya na kukosa shukurani. Kauli ya serikali ni kauli ya chombo kinachoendelea kukosa uhalali wa kuongoza taifa. Ni kauli ya kukata tamaa. Ni kauli hatari sana dhidi ya Watanzania waliojitolea damu kulinda uhuru wa nchi yao.”

Zitto alifafanua kuwa serikali katika kauli yake haitaji kabisa kwamba toka Uhuru watu wa Mtwara na Lindi wamekuwa wachangiaji wakubwa sana katika uchumi wa taifa kupitia zao la korosho.
Alisema takwimu za uzalishaji wa korosho zinaonyesha kwamba kuanzia mwaka 1965 mpaka 2011 zimeliingizia taifa fedha za kigeni jumla ya dola za Kimarekani bilioni 4.58. Katika mwaka wa uchumi unaoishia Novemba 2012, korosho imeliingizia taifa jumla ya dola za Kimarekani 151 milioni. Katika mwaka 2011 zao hili liliingiza dola milioni 130 wakati pamba iliingiza dola 53 milioni tu.
Zitto alihoji kuwa tunaipima kwa fedha? Uroho wa gesi asilia kuzalisha umeme wa kufurahisha walalaheri asilimia 14 nchini ndio inaifanya serikali kusahau kabisa kujitoa muhanga kwa watu wa Mtwara katika kulinda uhuru wa taifa letu?
Kwamba serikali kusema lazima bomba lije Dar es Salaam kwa sababu ndiyo inazalisha asilimia 80 ya mapato ya serikali ni uongo na aibu serikali kujitetea kwa uongo.
“Dar es Salaam ni kituo tu cha kukusanyia mapato ya serikali. Uzalishaji mkubwa wa nchi yetu wenye kuzalisha kodi unafanyika nje ya Dar es Salaam. Walipa kodi wakubwa wengi ofisi zao kuu ziko Dar es Salaam lakini uzalishaji wao unafanyika nje ya Dar es Salaam.
Serikali itoe orodha ya walipa kodi wakubwa 100 tuone uzalishaji halisi wa mapato hayo unafanyika wapi,” alihoji. Zitto alisistiza kuwa maandamano ya watu wa Mtwara ni kielelezo tosha kwamba watu wa mikoa ya Lindi na Mtwara wamechoshwa na longolongo za serikali.
Alisema kuwa watu wa Mtwara na Lindi wameona historia ya bomba la Songosongo. Hata kodi ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (asilimia 0.3) ilikuwa inalipwa na Halmashauri ya Manispaa Ilala na kampuni ya Pan Africa Energy.
Lipumba, Mbatia wanena
Akizungumza na gazeti hili, Profesa Lipumba alisema anashindwa kumwelewa Waziri Muhongo, hajui hali halisi ya maeneo ya Watanzania, kama hawezi kusema gesi iko maeneo gani katika mikoa ya Tanzania, basi ni profesa wa ajabu kidogo.
Alifafanua kuwa anashindwa kumwelewa kwani anapingana na sera ya serikali ambayo yeye mwenyewe ni waziri.
Alisema kuwa kama gesi ilipoanza kuchimbwa Songosongo likajengwa bomba dogo la nchi 12 kusafirisha gesi chini ya bahari toka Songosongo hadi Somanga na bomba la nchi 14 lilijengwa toka Somanga hadi Dar es Salaam.
“Uwezo wa mabomba haya ni mdogo ukilinganisha na gesi inayopatikana Songosongo na mahitaji yake kwa shughuli ya kufua umeme na kutumia viwandani,” alisema.
Alisema kuwa mpango huu ulikubaliwa na serikali na ukaingizwa katika Mpango Kabambe wa Taifa wa kufua na kusambaza umeme, kwamba mradi huo wa kufua umeme MW 300 Mtwara ulipangwa uwe umekamilika mwaka huu wa 2012.
Lipumba aliongeza kuwa wananchi wa Mtwara wanahitaji kujua kwa nini serikali haikutafuta njia mbadala ya kugharamia mpango wa kufua umeme na kuiunganisha Mtwara na gridi ya taifa.
Naye Mbatia akizungumza na waandishi wa habari alisema kuwa anashangazwa na viongozi wa CCM wanaposhindwa kuwa na sauti moja ya kusimamia rasilimali za taifa na hivyo kuparaganyika na kupishana kauli katika suala la gesi.
“Hatuhitaji viongozi wa kuuliza Watanzania tunataka nini, Watanzania wote tunataka kushirikishwa hasa katika masuala ya rasilimali ya gesi, maumivu ya mikataba mibovu katika sekta ya madini na sekta nyingine imetuchosha,”alisema.
Naye Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Helen Kijo-bisimba, pamoja na Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania, Ussu Mallya, walisema wananchi hawana tatizo isipokuwa serikali haijawashirikisha kwani wanajua kuwa mikoa yao imeachwa nyuma muda mrefu bila maendeleo.

No comments:

Post a Comment