Pages


Photobucket

Tuesday, January 1, 2013

VIGOGO WALIOLIA, NA WALIOCHEKA 2012

BAADHI ya vigogo wa kisiasa hawatasahau yaliyowapata mwaka jana kutokana na mabadiliko makubwa yaliyoigusa medani hiyo na kusababisha kuanguka ama kwa kura au kung’olewa katika nafasi walizokuwa wakizishikilia.
Wakati baadhi wakiugulia kwa machungu hayo, kwa upande mwingine lipo kundi la wale wanaosherehekea neema iliyowajia mwaka huohuo, baada ya nyota zao kung’ara kisiasa na kujikuta wakikwaa nafasi za uongozi, pengine ambazo hawakuzitarajia.
Miongoni mwa matukio yaliyowatikisa wanasiasa ni hatua ya Rais Jakaya Kikwete kupangua Baraza la Mawaziri, kutenguliwa kwa baadhi ya matokeo ya chaguzi za wabunge na uchaguzi wa ndani wa CCM ambao uliwaweka kando baadhi ya vigogo wa chama hicho.
Kadhalika, yapo matukio yenye sura ya kipekee ambayo yanawagusa wanasiasa kama Godbless Lema ambaye alianguka kisiasa kwa ubunge wake kutenguliwa na Mahakama Kuu, Kanda ya Arusha mwanzoni mwa mwaka jana, lakini akaibuka tena shujaa baada ya kurejeshewa nafasi hiyo na Mahakama ya Rufani, Desemba 2012.
Tukio kubwa ambalo lilitikisa siasa za Tanzania ni lile la mabadiliko katika Baraza la Mawaziri ambayo yaliwaweka kando mawaziri sita ambao walikuwa wakiziongoza wizara nyeti zinazosimamia rasilimali za nchi na huduma za afya na uchukuzi.
Waliong’olewa ni Mustafa Mkulo (Fedha), William Ngeleja (Nishati na Madini), Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii), Omari Nundu (Uchukuzi), Dk Cyril Chami (Viwanda na Biashara) Dk Haji Mponda (Afya na Ustawi wa Jamii). Pia panga hilo liliwakumba waliokuwa Naibu Mawaziri, Dk Lucy Nkya (Afya na Ustawi wa Jamii) na Dk Athuman Mfutakamba (Uchukuzi).


Kuanguka kwa Mkulo, Ngeleja na Maige kulitokana na taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) iliyozihusisha wizara zao na ufisadi. Dk Mponda na Dk Nkya, waling’olewa kutokana shinikizo la madaktari ambao walifanya mgomo uliotikisa sekta ya afya nchini.
Kwa upande wake, Nundu naibu wake, Dk Mfutakamba waling’olewa kutokana na kashfa ya ujenzi wa gati bandarini ambao uliwagawa kiasi cha kutofautiana bungeni, wakati Dk Chami naye aliponzwa na ugomvi na aliyekuwa naibu wake, Lazaro Nyalandu. Hata hivyo Nyalandu alipona baada ya kuhamishiwa Wizara ya Maliasili na Utalii.
Walioula
Mabadiliko hayo yalikuwa neema kwa wateule wapya wakiwamo wale ambao hawakuwahi kuwa wanasiasa kama ilivyo kwa Profesa Sospeter Muhongo ambaye aliteuliwa kuwa Waziri wa Nishati na Madini.
Profesa Muhongo alipewa naibu wawili; George Simbachawene (Nishati) na Stephen Masele (Madini) ambao walikuwa wabunge.
Wabunge wengine walioula ni Dk William Ngimwa ambaye aliteuliwa kuwa Waziri wa Fedha na kupewa naibu wawili ambao nao hawakuwa katika duru za kisiasa; Saada Mkuya Salum na Janeth Mbene. Ni wakati huohuo ambao Mwenyekiti wa NCCR -Mageuzi, James Mbatia aliteuliwa na Rais kuwa mbunge.
Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment