Pages


Photobucket

Thursday, August 8, 2013

KATIBA : Dk Mvungi alazimika kuhubiri dini Misenyi



 
Na Editha Majura, Mwananchi 
Wajumbe 96 wa Mabaraza ya Katiba, Wilaya ya Misenyi mkoani Kagera, wamekutana kujadili Rasimu ya Katiba Mpya, kwa lengo la kuiboresha, kazi itakayodumu kwa siku tatu.
Akifungua mkutano huo jana, Afisa Utumishi wa wilaya hiyo, Donard Nssoko, alitaka wajumbe hao watoe maoni kwa niaba ya wananchi  ili Katiba ijayo iwe yenye maslahi kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Katika hali inayoashiria kuwa, tume imedhamiria kudhibiti wajumbe wa mabaraza hayo,wasiingize maoni yanayotokana na shinikizo la makundi ya kisiasa, kidini na kiuana harakati, mbinu mbalimbali za kubadili fikra za wajumbe hao zilitawala ufunguzi wa mkutano huo.
Mwenyekiti wa Tume mkoani humo, Dk, Sengondo Mvungi aligeuka muhubiri alipokuwa akielekeza namna wajumbe wanavyotakiwa kutekeleza jukumu hilo, baada ya maelezo yake kulenga kujenga hofu ya Mungu ndani ya wajumbe.
“Mmetumwa na wananchi siyo mjigeuze tume, bali mboreshe maoni yao kwa kuandika kila kitakacholetwa na mjumbe, ili kikafanyiwe kazi na tume; kushiriki kwenu kuunda sheria kuu kwa Watanzania siyo suala la kibinadamu, bali Mungu amekushirikisha ufanye kazi hiyo kwa niaba yake,” alieleza Dk, Mvungi
Dk. Mvungi aliwataka watambue kuwa hawapo kutumiwa na makundi fulani, kuchakachua kwa kubadili maoni ya wananchi yaliyo katika rasimu, bali kuyaboresha na kwamba kama ilivyo kwa imani za Kikristo na Kiislamu, kwamba wanaoshiriki kujenga Kanisa au Msikiti wamebarikiwa.
Alisema kidunia, wanaoshiriki kuunda Katiba ambayo ni sheria kuu ya nchi, wamebarikiwa na kwamba kinyume na baraka za Mungu ni laana, hivyo akaasa wanapotekeleza jukumu hilo, wajitambue kuwa wanamtumikia Mungu kwa ajili ya watu wake wa Tanzania.
“Mimi siyo Padri, Askofu wala Sheikh nakuelekeza haya, ili ufahamu kuwa usipokuwa mwaminifu kwa Mungu na taifa lako katika hili, hutapata nafasi ya kujitetea mbele za Mungu, msije mkasema hatukujua kuwa kazi ya kutunga Katiba ni ya Mungu; ukikosea utahukumiwa,” Dk. Mvungi alieleza
Mjumbe wa Sekretalieti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Marlin Komba kabla ya kufungua mkutano huo, alitoa karatasi kwa kila mjumbe ili iandike wadhifa na sifa yake katika jamii aliyotoka. Vikakusanywa na kuhifadhiwa kwenye bahasha moja.
“Vyeo na sifa zenu zimehifadhi kwenye bahasha hii, ukumbini mmebaki wajumbe wa mabaraza ya Katiba, mtakaoboresha rasimu ya Katiba ili ipatikane Katiba itakayokidhi mahitaji ya Watanzania siyo kwa maslahi ya dini, siasa au uanaharakati,” Komba alieleza
Kama hiyo haitoshi, mwisho wa maelekezo ya tume, Komba aliongoza mabaraza hayo kuimba ubeti mmoja wa wimbo wa taifa, akihimiza kuzingatia umuhimu wa kumshirikisha Mungu na kuzingatia utaifa katika kazi wanayotakiwa kufanya.
Baadhi ya wananchi walionekana kupendelea zaidi makundi fulani ya wananchi, mambo ambayo yanaonekana wazi kwamba yanaweza kuifanya katiba isizae matarajio ambayo wengi wanayo ya kuwepo kwa katiba iliyo safi kwa wote.

No comments:

Post a Comment